Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Tuesday, June 15, 2010

SHIRIKA LA HAKI ZA BINADAMU LAWACHONGEA WANASIASA KWA WAKULIMA

Na Thobias Mwanakatwe, Rungwe



SHIRIKA la Kinga za Binadamu na Haki za Raia Tanzania , limewapa somo wakulima wa chai wa Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya kuwahoji wanasiasa watakaokwenda kwao kuomba ridhaa ya kutaka wachaguliwe kuwa wabunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu wamewafanyia nini walipokuwa madarakani katika kuwatafutia soko la kuuzia mazao yao .



Shirika hilo limesema hayo jana wakati wa mkutano na wakulima wa vijiji vya Itula,Bugoba,Katundulu,Kibatata na Ndubi ulioitishwa na Chama cha Ushirika wa Wakulima wa Chai Rungwe (RUTECO) kujadili matatizo yanayowapata wakulima kutokana na bei ndogo isiyo na manufaa wanayouzia chai kwa mwekezaji wa Kiwanda cha Katumba cha Watco.



Makamo Mwenyekiti wa Shirika hilo, Joseph Mngumi, alisema wakulima wa chai wilaya ya Rungwe kwa muda mrefu wamekuwa wakipata tabu ya kukosekana na soko la ushindani la kuuza chai yao na hivyo kuwalazimu kuuza chai kwa mwekezaji pekee wa kiwanda cha kusindika chai cha Katumba kwa bei ambayo haiwanufaishi.



“Mwaka huu ni mwaka wa uchaguzi wapo wanasiasa watakaokuja kwenu na kuomba muwachague kuwa wabunge wenu, nawaombeni wakija muwahoji je walipokuwa madarakani wamesaidiaje katika kuwatafutia soko la uhakika na la ushindani la zao chai,”alisema Mngumi.



Mngumi alisema kutokana na wakulima kuuza chai yao kwa bei ya hasara, wameshinda kuboresha maisha yao ikiwepo kushindwa kujenga nyumba bora na kwamba wakati umefika kwa wakulima kuungana kutetea maslahi yao ambapo shirika hilo litawaunga mkono kisheria.



Kwaupande wake Mkurugenzi wa Shirika hilo, Jelard Mwakalukwa, alisema wakulima wa chai wana haki ya kuhoji waendelee kuuza chai kwa bei ya hasara na kwamba hata hivyo tatizo lililopo ni kwenye mkataba ambao haujawekwa wazi hivyo imekuwa ikitoa fursa kwa mwekezaji wa kiwanda cha Katumba kuwa mnunuzi pekee wa chai katika wilaya ya Rungwe.



Mwakalukwa alisema Rais Jakaya Kikwete alimteua Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Jackison Msome kwasababu ana imani naye hivyo ni kwanini anashindwa kuyapatia ufumbuzi malalamiko ya wakulima wa chai ambao kwa muda mrefu wanalalamika kuwa bei ya Sh.160 kwa kilo wanayomuuzia mwekezaji wa kiwanda cha Katumba haiwanufaishi.



“Rais Kikwete alimteua DC Rungwe kwasababu ana imani naye, kwa hiyo kama DC anashindwa kuwakutanisha wakulima ambao ni wanachama wa Chama cha Ushirika wa Wakulima wea Chai Rungwe (RUTECO) na wale Umoja wa Wakulima wWadogo wa Chai Rungwe (RSTGA) hivyo basi kwanini sisi tusimweleze Rais kwamba hatuna imani naye,”alisema Mwakalukwa na kushangiliwa na wakulima.



Naye Mwenyekiti wa Chama cha Ushirika wa Wakulima wa Chai Rungwe (RUTECO), Timoth Kaswaga, alisema wakulima wa chai wanahoji kwanini serikali imekuwa ikisisitiza uwekezaji wa ushindani lakini wanashangaa serikali hiyo hiyo inakataa kutoa kibali kwa mwekezaji wa Kampuni ya Mohamed Enterprises (T) Limited (METL) ili aanze kununua chai kwa bei ya ushindani.

Kaswaga alisema kutokana na tabu wanayopata, wakulima wa chai katika vijiji 104 vinavyolima zao hilo wilayani Rungwe watamuunga mkono mwanasiasa ambaye wataona anawasaidia katika kuhakikisha bei ya chai imeongezwa ili wakulima waanze kunufaika na kilimo cha zao hilo .


Hivi karibuni Meneja Mwendeshaji wa Mashamba ya Chai ya Kampuni ya Mohamed Enterprises (T) Limited,George Mwamakula alisema tangu mwaka jana kampuni yake ilipeleka maombi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe kutaka wapewe kibali cha kununua chai kama sheria inavyoelekezwa lakini wamekuwa wakipewa ahadi ambazo hazitekelezwi hadi sasa.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...