Marquee

Pata habari za Jamii,Biashara,Burudani na michezo!!

tangazo

Tuesday, February 11, 2014

Mabingwa Airtel Rising Stars wasichana wajazwa noti




 TIMU ya wasichana ya Tanzania imekabidhiwa zawadi ya Sh milioni 16 baada ya kutwaa ubingwa wa michuano ya vijana walio chini ya umri wa miaka 17 ya Kimataifa ya Airtel Rising Stars iliyofanyika Septemba mwaka jana nchini Nigeria.

Timu hiyo ilitwaa taji hilo baada ya kuifunga Kenya bao 1-0 lililofungwa na Donisia Daniel katika fainali hiyo. Akipokea fedha hizo jana (Februari 10, 2014) Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA), Msanifu Kondo alisema.

wanaishukuru Kampuni ya Airtel kwa kutimiza ahadi yao ya zawadi ya fedha hizo na tayari wamezikabidhi kwa makocha na wachezaji wa timu hiyo.

Alisema kila mchezaji amepewa Sh 850,000 wakati kocha mkuu wa timu hiyo Rogasian Kaijage amepewa Sh milioni moja na laki mbili na kocha msaidizi amepewa Sh milioni moja.  “Tunawashukuru Airtel kwa kutoa fedha hizo za zawadi kwa timu hii na sisi tumewakabidhi wahusika,” alisema.

Kwa upande wake Afisa Uhusiano wa Airtel Tanzania Jane Matinde alisema wao kama wadhamini wa mashindano hayo wametimiza ahadi yao kwa kukabidhi fedha hizo kwa mabingwa hao.

“Kwa niaba ya Airtel Tanzania tunaipongeza timu ya wasichana ya Tanzania kwa kutwaa ubingwa huo, lakini pia tumetekeleza ahadi yetu ya kukabidhi zawadi, kama mnavyofahamu kampuni yetu imekuwa mstari wa mbele katika kusaidia mambo ya kijamii lakini pia michezo ikiwemo soka kupitia michuano ya vijana ya Airtel Rising Stars kwa kushiriki na klabu ya Manchester United,” alisema.

Mohamed Mharizo
Ofisa Habari wa DRFA

Februari 11, 2014

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...